1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Iran kuwaachia wafanyakazi wa meli inayohusishwa na Israel

Tatu Karema
27 Aprili 2024

Iran imesema kuwa wafanyakazi waliokamatwa wa meli iliyokuwa na bendera ya Ureno aina ya MSC Aries inayohusishwa na Israel, wameruhusiwa kuwasiliana na balozi zao nchini humo na wanatarajiwa kuachiwa huru.

https://p.dw.com/p/4fFbf
Meli ya MSC Aries ikiwa katika bandari ya  Los Angeles Long Beach
Meli ya MSC Aries (kulia) ikiwa katika bandari ya Los Angeles:18.10.2021Picha: Damian Dovarganes/AP/picture alliance

Haya yameripotiwa leo na vyombo vya habari vya Iran vikinukuu kauli ya Waziri wa mambo ya nje wa Iran Hossein Amirabdollahian. Wakati wa mazungumzo kwa njia ya simu, Amirabdollahian amemwambia mwenzake wa Ureno Paulo Rangel kwamba suala la kibinadamu la kuachiliwa kwa wafanyakazi wa meli hiyo ni la umuhimu mkubwa kwao.

Soma pia:Iran yaikamata meli ya Israel licha ya onyo la Biden

Amirabdollahian pia amenukuliwa na vyombo hivyo vya habari akisema kuwa wafanyakazi hao watawasilishwa kwenye balozi zao nchini humo. Hata hivyo ripoti hizo hazikueleza ni lini hatua hiyo itakapochukuliwa.

Wizara ya mambo ya nje ya Iran imesema kuwa meli hiyo iliyokuwa na abiria 25, ilikamatwa Aprili 13 katika mlango wa bahari wa Hormuz kwa kukiuka sheria za baharini na kwamba hakuna shaka ilihusishwa na Israel.